Aibu: Riadha miaka 20 medali saba tu

Nuzulack Dausen
March 29, 2017

Imani Makongoro, Mwananchi
[email protected]

Dar es Salaam. Kwa takriban miaka 20 sasa, Tanzania imekuwa ikisuasua katika riadha, licha ya Shirikisho la Riadha nchini (RT) kupeleka timu kwenye mashindano mbalimbali ya kimataifa ikiwemo Michezo ya Olimpiki, Afrika, Madola na ubingwa wa dunia na mbio za nyika.

Takwimu za Shirikisho la Riadha la Kimataifa (IAAF) zinaonyesha kuwa tangu mwaka 1997 hadi Machi mwaka huu, wanariadha 130 waliwakilisha nchi katika mbio mbalimbali, huku wakirudi na medali za kimataifa saba pekee.
K
ati ya medali hizo saba, nne za dhahabu zilibebwa na Restituta Joseph, Samson Ramadhan, Fabiano Joseph na Alphonce Simbu.
Dhahabu hizo zilianza kupatikana mwaka 2001 baada Restituta, ‘binti’ wa Singida, kushinda katika Mbio za Nyika za dunia. Joseph aliitwaa dhahabu katika mbio za dunia mwaka 2007, Ramadhan (Jumuiya ya Madola, 2006 na Simbu aliyeshinda mashindano ya Standard Chartered Mumbai Marathon Januari mwaka huu.

Mbali na dhahabu, wanariadha wa Tanzania waliwahi kushinda medali mbili za fedha na shaba moja kiwango ambacho ni kidogo ikilinganishwa na medali walizovuna Kenya ndani ya kipindi hicho.

Pamoja na wingi huo wa wanariadha, uchambuzi wa Mwananchi umebaini kuwa robo tatu ya wanamichezo hao wamekuwa wakitoka kwenye mikoa miwili tu ya Singida na Manyara jambo linaloonyesha kuwa mikoa mingine hakuna uwekezaji wa kutosha katika mchezo huo.
Kati ya wanariadha hao, 52 ni wazaliwa wa Singida na 40 wa Manyara huku 38 waliosalia wakitokea mikoa ya Arusha, Dodoma, Mara na Mbeya huku Dar es Salaam yenye wakazi takriban milioni tano, ikikosa kabisa uwakilishi katika kipindi hicho.

Manyara na Singida hazijawa kitovu cha riadha nchini kwa bahati mbaya. Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wetu katika mikoa hiyo, umebaini kuwa mchezo huo ni sehemu ya maisha ya wakazi wa mikoa hiyo huku baadhi ya familia zikiwa tayari kuwapeleka watoto wao katika vituo maalumu kukuza vipaji vyao.

Tofauti na mikoa mingine kama Dar es Salaam, ndani ya Manyara na Singida hasa vijijini ni nadra kuwaona watoto wakicheza mpira wa miguu badala yake sehemu kubwa hushiriki michezo ya kukimbia na kulenga shabaha.

Nuzulack Dausen

Nuzulack Dausen ni Mkuu wa dawati la habari za takwimu wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti. Mwaka 2015 alishinda tuzo ya Mwandishi bora wa habari za Uchunguzi kwa upande wa magazeti zinazotolewa na Baraza la Habari Tanzania (MCT). Amejikita zaidi katika habari za biashara, uchumi, teknolojia na data.

MWANANCHIDataLab by Code for Tanzania