Ripoti: Uchoyo waanza kuwaandama Watanzania

Nuzulack Dausen
September 11, 2017

*Ni rahisi kwa Watanzania kukupatia fedha lakini siyo kupoteza muda kukuhudumia kama una shida

[email protected]

Dar es Salaam. Tanzania imeporomoka nafasi sita katika utafiti wa ukarimu duniani ikiwa ni mwaka mmoja baada ya kufanya vizuri jambo linaloonyesha kuwa Watanzania wameanza kuwa mkono wa birika katika kuchangia watu wenye uhitaji.

Ripoti mpya ya ukarimu ya mwaka 2017 iliyotolewa mwishoni mwa wiki iliyopita inabainisha sasa Tanzania inashika nafasi ya 63 duniani kutoka 57 mwaka jana nyuma ya majirani Kenya na Uganda katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Katika ripoti hiyo ya kila mwaka, inayoandaliwa na asasi ya kiraia ya kimataifa kutoka Uingereza ya Charities Aid Foundation (CAF), inaonesha kuwa Tanzania imeanguka katika vipengele viwili kati ya vitatu ambavyo hutumika kupima ukarimu wa watu wa nchi husika.

Mwaka jana, Tanzania ilifanya vyema katika utafiti huo baada ya kufanya vyema katika vipengele vyote vya ‘kumsaidia usiyemjua’, kuchangia fedha’ na ‘kujitolea muda kwa ajili ya kuwasaidia wale wenye uhitaji’.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya nane, ni rahisi kwa Watanzania kukupatia fedha lakini siyo kupoteza muda wao kukusaidia au kukuhudumia iwapo hawakufahamu.

Katika ripoti ya mwaka huu, Tanzania inashika nafasi ya 110 katika kipengele cha kujitolea muda kwa wenye uhitaji na nafasi ya 60 kati ya 138 zilizofanyiwa utafiti duniani katika kipengele cha kusaidia wageni wasiofahamika.

Ni kipengele kimoja tu cha kujitolea fedha ambacho Tanzania imepaa kwa nafasi 13 kutoka nafasi ya 49 mwaka jana hadi nafasi ya 36 mwaka huu ikiwa juu ya Uganda, Rwanda na Sudan ya Kusini.

Hii ni kinyume na majirani zao wa Kenya ambao wanashikilia nafasi ya pili ulimwenguni kwa kujitolea muda kwa wenye uhitaji na nafasi ya nne kwa kumsaidia mgeni wasiyemjua. Kenya ni nchi ya tatu duniani kwa ukarimu.

Hata hivyo, ripoti hiyo ya utafiti huo uliofanywa mwaka jana inabainisha kuwa licha ya ukarimu kushuka kwa ujumla duniani mwaka jana, bado Afrika imefanya vyema baada ya wastani wa ukarimu kupanda kwa kila kipengele.

“Afrika mwaka huu imeenda kinyume na mwenendo wa dunia na ndiyo bara pekee lililoshuhudia kupanda kwa tabia ya kujitolea katika vipengele vyote vitatu itakapolinganishwa na wastani wa ukarimu kwa miaka mitano,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo.

Myanmar ndiyo nchi yenye ukarimu zaidi duniani kwa mwaka wa nne mfululizo ikifuatiwa na Indonesia na Kenya.

Utafiti huo ulifanywa katika nchi 138 uliwauliza baadhi ya watu walioteuliwa kuwa sampuli kuwa ni mara ngapi huwasaidia watu wasiowajua, kuchangia fedha na kujitolea muda wao kwa wasiojiweza ili kupima kiwango cha ukarimu wao.

“Ili kuongeza tabia ya kujitolea miongoni mwa watu ulimwenguni, serikali zote zinatakiwa kuhakikisha asasi za kiraia zinadhibitiwa kwa haki na kwa uwazi, zirahisishe mazingira ya watu kujitolea na kutoa motisha pale inapobidi,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo na kuongeza;

“Pia, zihamasishe uwepo wa asasi za kiraia kama sauti huru za maisha ya watu kuheshimu haki za taasisi zisizo za kifaida kuzungumzia masuala ya msingi ya kitaifa.”

 

Nuzulack Dausen

Nuzulack Dausen ni Mkuu wa dawati la habari za takwimu wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti. Mwaka 2015 alishinda tuzo ya Mwandishi bora wa habari za Uchunguzi kwa upande wa magazeti zinazotolewa na Baraza la Habari Tanzania (MCT). Amejikita zaidi katika habari za biashara, uchumi, teknolojia na data.

MWANANCHIDataLab by Code for Tanzania