Uhaba wa maji safi na salama unavyotishia maisha ya wanavijiji wilayani Nachingwea

Nuzulack Dausen
October 4, 2017

Nuzulack Dausen, Mwananchi [email protected]

Takriban mita 700 kusini mwa barabara ya Nachingwea-Liwale pembezoni mwa kisima kifupi cha wazi katika Kijiji cha Lionja B, Severine Conrad (16) anakunywa maji kwa kutumia kidumu kidogo cha lita tatu kilichokatwa mdomoni.

Maji anayokunywa Conrad, anayesoma kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari Lionja wilayani Nachingwea mkoani Lindi, yanatoka katika kisima hicho kifupi cha udongo kilichochimbwa kwenye shamba la miwa ambalo huwa ni eneo oevu wakati wa masika.

“Siwezi kuhofia kuumwa kwa kunywa maji haya hata kama ni machafu kwa kuwa nimeyazoea. Haya maji ndiyo tunayokunywa kila siku na hakuna mengine,” anasema Conrad licha ya kukiri kufundishwa shuleni umuhimu wa kuchemsha maji.

Conrad siyo mkazi pekee wa eneo hili anayekunywa maji machafu bila ya kuyatibu. Wananchi wengi wanakunywa maji hayo kutokana na uhaba wa vyanzo vya maji safi na salama jambo linalowaweka katika hatari ya kushambuliwa na magonjwa ya tumbo mara kwa mara na kudhorotesha afya zao.

Katika vijiji vya Lionja A, Lionja B, Litandamtama, Nangunde, Namikango A na Namikango B vyanzo vyote vya maji si safi na salama kasoro kisima kimoja tu cha pampu ya mkono.

Kisima hicho cha pampu nacho kimejengwa Juni mwaka huu katika Kitongoji cha Mayaka katika Kijiji cha Lionja A na asasi ya kiraia ya GAIN ambacho tayari kimeanza kuzidiwa na msongamano wa watu kwa kuwa hakina maji ya chumvi kama vingine.

Mkazi wa Kijiji cha Lionja A wilayani Nachingwea, Mkoa wa Lindi akichota maji kwenye kisima pekee cha maji safi na salama kilichopo katika kitongoji cha Mayaka kijijini hapo. Picha zote na Nuzulack Dausen
Mkazi wa Kijiji cha Lionja A wilayani Nachingwea, Mkoa wa Lindi akichota maji kwenye kisima pekee cha maji safi na salama kilichopo katika kitongoji cha Mayaka kijijini hapo. Picha zote na Nuzulack Dausen

Kisima hicho kinahudumia watu zaidi ya 3,200 wa kijiji hicho, kiwango ambacho ni kikubwa mara 12 ya utaratibu uliopangwa na Sera ya Taifa ya Maji ya mwaka 2002 inayoagiza kituo kimoja cha maji kuhudumie wastani wa watu 250.

Visima vingi katika vijiji hivi ni vya udongo vilivyowazi na vingi havizidi urefu wa kati ya futi sita hadi 10. Sehemu kubwa vimezungukwa na vichaka na vipo mbali na makazi huku baadhi wakilazimika kusafiri zaidi ya kilomita tano kufuata maji katika visima hivyo.

 

Ndani ya visima hivyo kama cha Kwa Bakari Libea katika Kijiji cha Litandamtama kuna takataka zimetumbukia, vyura wanaogelea na kukimbia pale mtu anapoingiza kopo la kuchotea maji. Maji yamebadilika na kuwa rangi ya kutu.

“Unashangaa takataka za miti na fimbo, kuna wakati wanafia panya humu ndani na tunachota tu. Hata kama tukihofia kuathirika tutaenda kuchota maji wapi ambako siyo mbali na nyumbani?” anasema Asia Ibu, mkazi wa Kijiji cha Litandamtama.

Ni Kijiji cha Lionja A pekee kilichobahatika kuwa na visima vifupi 12 vilivyojengwa na saruji bila kufunikwa ambavyo maji yake ni ya chumvi na Lionja B chenye kisima kimoja kilichojengewa na saruji.

Utaratibu uliopo ni kwamba kila mchotaji anakuja na kichoteo chake chenye kamba ndefu anachokitumbukiza kisimani ili mradi awahi kupata huduma hiyo muhimu kwa mwanadamu.

Sehemu kubwa ya wachota maji katika kisima maarufu cha Chengo wanavifaa kukuu kama vibuyu na vidumu vya lita tano vilivyokatwa midomoni ili vichote maji kwa wingi. Ni wachache wanavifaa vya kisasa kama ndoo mpya za plastiki za lita 10.

Kisima cha Chengo kilichopo Lionja A wakati wa kiangazi kuanzia Septemba hadi Desemba kwa mujibu wa diwani wa Lionja, Joachim Mnungu kinahudumia vijiji vya kata tatu vikiwemo Litandamtama, Lionja B, Namikango A, Namikango B, Nangunde, Nalengwe na Naulingo kwa kuwa kinadumu misimu yote na kina maji yenye chumvi kidogo kuliko vingine.

“Kupata maji ya kunywa ni shida. Kuna kipindi cha kiangazi tunatoka asubuhi kwenda Chengo au mabondeni na kurudi jioni kutokana na foleni ya wachotaji,” anasema Calcansia Tindwa anayeishi katika Kijiji cha Lionja B.

Ili afike katika Kisima cha Chengo kutoka nyumbani kwake, Calcansia analazimika kutembea umbali wa takriban kilomita nne.

Pamoja na kwamba maji hayo si salama, Calcansia aliyekutwa akichota maji kisimani akiwa na mwanaye wa miezi mitatu, anasema maji hayo huwanywesha pia watoto wao wadogo bila kuchemsha au kutia dawa za kutakatisha.

Wananchi hao wanapata shida ya maji licha ya lengo namba 4.4 la Sera ya Taifa ya Maji ya mwaka 2002 kutaka wakazi wa vijijini wapate angalau lita 25 za maji safi na salama kwa mtu mmoja kwa siku na ndani ya mita 400 yalipo makazi yao.

Uelewa duni wa kutibu maji

Hata pamoja na kwamba maji hayo yanaweza kutibiwa kuua vijidudu vinavyosababisha magonjwa ya tumbo, sehemu kubwa ya wakazi hao hawachemshi wala kutakatisha maji na dawa kama ‘Waterguard’.

“Tanakunywa tu hivyo hivyo bila ya kuchemsha. Hakuna mtu hapa mwenye utaalamu huo wa kuchemsha maji ya kunywa,” anasema Abas Mussa (78).

Hata hivyo, wapo wanaojua umuhimu wa kuchemsha maji hususan akina mama ambao hupatiwa elimu hiyo kliniki kama Calcansia, lakini hawachemshi kwa kile wanachodai ni ‘utamaduni’ wao.

“Huu ni utamaduni wetu kunywa maji bila kuchemsha na sisi tumekuta kwa wazee wakifanya hivyo tangu zamani na wote tunatumia maji hayo hayo,” anasema Calcansia.

Ukiachana na ukosefu wa elimu ya kuchemsha maji, bado upatikanaji wa dawa za kusafisha maji katika vijiji hivi ni shida. Uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa hakuna duka linalouza dawa hizo wala zahanati ambayo inawapatia bure.

Madhara ya maji machafu

Matumizi ya maji yasiyo safi na salama yanawagharimu wakazi wa vijiji hivyo kiasi cha baadhi yao kukumbwa na magonjwa ya kuhara mara kwa mara na kusababisha wasifanye shughuli zao za uzalishaji.

Mkazi wa Kijiji cha Lionja A, Fabiola Nnali (48) anasema ni kawaida kwa familia yao kukumbwa na magonjwa ya kuharisha na wakienda zahanati au hospitali madaktari huwa wanawaambia hali inatokana na kunywa maji machafu.

“Kuharisha siyo jambo geni, mwaka jana niliumwa sana ugonjwa wa kuhara damu ilibidi nienda hospitali Mnero kutibiwa. Kwa shida hizi tunaomba Serikali itusaidie kutujengea visima vizuri angalau tupate maji safi na salama,” anasema Fabiola.

Siyo wote wanaoumwa kama Fabiola wanaenda kutibiwa hospitali. Baadhi kama Fatuma Ismail (75) huwa anatumia mitishamba au kununua dawa katika maduka ya dawa muhimu kujitibu.

Picha ikimuonyesha mkazi wa Kijiji cha Lionja B katika Wilaya ya Nachingwea mkoani Lindi akinywa maji ya kisimani kutoka kwa mwenzake hivi karibuni bila ya kuyachemsha.
Picha ikimuonyesha mkazi wa Kijiji cha Lionja B katika Wilaya ya Nachingwea mkoani Lindi akinywa maji ya kisimani kutoka kwa mwenzake hivi karibuni bila ya kuyachemsha.

Muuguzi wa Zahanati ya Lionja, Rehema Salumu anasema ni nadra kupokea watu wazima wanaoumwa magonjwa ya tumbo kwa kuwa baadhi huenda moja kwa moja kwenye hospitali ya misheni ya Mnero iliyopo kilomita zaidi ya 10 kutoka kijiji hapo.

“Watoto wa chini ya miaka mitano wanaoharisha ni wengi ambao kwa mwezi unaweza kupata sita na mkubwa mmoja tu. Hata hao watoto muda mwingine siyo kwa sababu ya maji machafu,” anasema Salumu.

Ugonjwa wa kuhara

Takwimu kutoka hospitali ya Mnero zinabainisha kuwa mwaka jana ugonjwa wa kuhara ulikuwa ni wa tatu kwa kuwa na wagonjwa waliolazwa wenye miaka zaidi ya miaka mitano, nyuma ya Malaria na magonjwa ya upumuaji, ukiwa na wagonjwa 109 kati ya 1,203 waliorekodiwa.

Kwa wagonjwa wasiolazwa wenye miaka zaidi ya miaka mitano, ugonjwa wa kuhara ulikuwa ni wa nne baada ya Malaria, homa ya mapafu na maambukizi ya njia ya mkojo (UTI).

Uhaba wa maji safi na salama vijijini unaikabili sehemu kubwa ya Halmashauri ya Nachingwea baada ya takwimu za Mkoa wa Lindi za hadi Juni mwaka huu kubainisha kuwa ni wakazi 45 tu kwa kila 100 wanaopata maji safi na salama ikilinganishwa na wastani wa kitaifa wa watu 72 kwa kila 100.

Uhaba huo umechangia wananchi wa wilaya hiyo kukabiliwa na magonjwa ya tumbo kama ilivyo katika vijiji vingi vya kata za Namikango na Lionja.

Takwimu kutoka ofisi ya Mganga Mkuu wa wilaya hiyo zinabainisha kuwa katika robo ya kwanza ya mwaka 2017 ugonjwa wa kuhara ulikuwa ni wa tatu nyuma ya Malaria na maambukizi ya njia ya mkojo (UTI), ukiwa na wagonjwa 3,028 waliobainika kuharisha huku zaidi robo wakiishiwa maji.

Wataalamu wa afya wanasema magonjwa ya tumbo kikiwemo kipindupindu yataepukika kwa uwepo wa maji safi na salama wakati wote na watu kusafisha mazingira yao ikiwemo kunawa mikono wanapotoka msalani.

“Wakati wa mvua wagonjwa ni wengi sana lakini wakati wa kiangazi wanapungua. Kuna wakati unakuta wodi nne wagonjwa wengi ni wa magonjwa ya kuharisha tu…na huenda hata takwimu zetu hizi ni ndogo kuliko uhalisia,” anasema Dk Leonard Shitanda, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Misheni ya Mnero.

Anasema magonjwa yanawapotezea watu muda mwingi wa kufanya kazi zao ndiyo maana huwa wanawapa elimu ya kutibu maji ili waepukane na magonjwa hayo ambayo yanaepukika kwa kufuata kanuni za usafi.

“Ila hakuna suluhu ya kudumu kama Serikali kusambaza maji safi na salama kwa vijiji vyote. Asasi za kiraia zenye uwezo ziangalie namna ya kusambaza dawa za kutibu maji kama Waterguard kama ilivyokuwa zamani ili kuwasaidia wananchi,” anasema.

Alipoulizwa wanatatua vipi wimbi la ugonjwa wa matumbo yanayotokana na maji machafu, Kaimu Mganga Mkuu wa halmashauri hiyo, Godfrey Mjungu anasema njia endelevu wanayotumia ni kutoa elimu ya kutibu maji kupitia kampeni ya usafi wa mazingira katika vijiji vyote 127.

Wataalamu wa afya wanasema magonjwa ya tumbo kikiwemo kipindupindu yataepukika kwa uwepo wa maji safi na salama wakati wote.
Wataalamu wa afya wanasema magonjwa ya tumbo kikiwemo kipindupindu yataepukika kwa uwepo wa maji safi na salama wakati wote.

“Huwa tunakusanya taarifa kila mwezi kujua kama elimu imefanya kazi na ni njia hii iliyosababisha kupunguza kesi za magonjwa ya tumbo japo bado yapo kidogo. Jambo kubwa ni kubadili tabia za wananchi wawe wasafi kwa kuwa wakati mwingine unakuta maji safi na salama yapo na bado wanaugua matumbo,” anasema Mjungu.

Nachingwea iliyokuwa na watu 169,327 mwaka 2012 kwa mujibu wa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi zilizochapishwa katika tovuti ya takwimu huru ya Hurumap Tanzania, ni wilaya ya mwisho mkoani Lindi kwa kuwa na watu wachache wanaopata majisafi na salama vijijini baada ya Ruangwa. Watu waliopo katika halmashauri hiyo ni sawa na moja ya tano ya watu wote katika mkoa huo wa kusini mwa Tanzania.

Ofisi ya mkurugenzi

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Arbogast Kiwale anakiri kuwepo kwa uhaba wa maji vijijini kuliko mijini akieleza kuwa hadi sasa asilimia 71 ya wakazi Nachingwea wanapata maji ikilinganishwa na asilimia 45 ya waishio vijijini.

“Kuna juhudi nyingi zinafanywa kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama ila miradi inatekelezwa kwa awamu. Tatizo kubwa ni kwamba vyanzo vikuu vya maji ni ardhini kwa kuwa hakuna mito ya kudumu kwa sababu mnaweza kuchimba visima mnakuta vyote maji hayafai kwa binadamu,” anasema.

Anasema mapema mwaka huu halmashauri kwa kushirikiana na kampuni ya utafiti wa madini walijenga kwa saruji visima vifupi 10 katika vijiji vya Lionja A na B na ndani ya miezi mitatu wataenda kuvifunika na kufunga pampu za maji ili kuvisitili na uchafu.

Kiwale anaeleza kuwa zimeshatengwa Sh585.6 milioni kwa ajili ya maji katika mwaka 2017/18 na baadhi ya maeneo yatakayonufaika ni Mituguru, Mitigera na Lupondera.

“Wakati tukiendelea kujenga visima na mabwawa kwenye baadhi ya vijiji vyenye shida ya maji safi na salama, tunawasihi wananchi kuvuna maji ya mvua wayatunze na wawe wanayechemsha ili kuepuka magonjwa ya tumbo,” anasema.

Nuzulack Dausen

Nuzulack Dausen ni Mkuu wa dawati la habari za takwimu wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti. Mwaka 2015 alishinda tuzo ya Mwandishi bora wa habari za Uchunguzi kwa upande wa magazeti zinazotolewa na Baraza la Habari Tanzania (MCT). Amejikita zaidi katika habari za biashara, uchumi, teknolojia na data.

MWANANCHIDataLab by Code for Tanzania