Yanga, Zanaco zinavyoisubiri mechi ya kisasi

Nuzulack Dausen
March 9, 2017

Fredrick Nwaka, Mwananchi

[email protected]

Dar es Salaam. Mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika baina ya Yanga na Zanaco utakaopigwa Jumamosi hii kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam utakuwa wa kisasi kwa Yanga ambayo miaka 11 iliyopita ilitolewa na Zanaco katika michuano hiyo.

Yanga na Zanaco zilikumbana kwenye mchezo wa raundi ya awali ya michuano hiyo mwaka 2006 ambapo licha ya watoto wa Jangwani kushinda mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa hapa nyumbani ililazwa mabao 2-0 kwenye mchezo wa marudiano. Kipigo hicho cha Yanga kiliifanya itolewe kwa jumla ya mabao 3-2.

Zanaco ambao ni mabingwa wa Zambia mwaka 2002, 2003, 2005, 2006, 2009, 2012 na 2016 wameshatua nchini kwa ajili ya mchezo na Kocha wake Mkuu, Mumamba Numba alinukuliwa na vyombo vya habari nchini Zambia kuwa kikosi chake kinaweza kupata matokeo ugenini.

“Mpira umebadilika sasa siamini kama kuna faida ya kucheza ugenini. Tunamjua Lwandamina kwa sababu tumefanya nae kazi, tunajua falsafa yake.Tunakwenda kucheza nao (Yanga) lakini sidhani kama Lwandamina amebadilisha falsafa yake,”alisema Numba.

Kikosi cha Zanaco mwishoni mwa mwaka jana. Picha na Mtandao.

Kabla ya kujiunga na Yanga mwezi Novemba, 2017 Lwandamina alifundisha klabu mbalimbali ikiwemo Zesco ambayo aliifikisha hatua ya nusu fainali ya klabu bingwa Afrika msimu uliopita.

Kuelekea mchezo huo Yanga itawakaribisha Amiss Tambwe na Donald Ngoma waliokuwa majeruhi lakini kuna hatihati ya kumkosa Juma Mahadhi na Geofrey Mwashiuya ambao waliumia kwenye mchezo wa Kombe la FA dhidi ya Kiluvya.

Aidha, beki mkongwe wa Yanga, Nadir Haroub ‘Canavaro’ ni mchezaji pekee aliyebaki kwenye kikosi cha Yanga kilichocheza na Zanaco 2006.

Soma: Yanga yamrudisha Lwandamina Zambia

Soma: Yanga yapitia njia ya AC Milan

Mchezo wa marudiano baina ya timu hizo, utapigwa wiki ijayo kwenye Uwanja wa Sunset mjini Lusaka ambapo mshindi atafuzu kucheza hatua ya makundi.

Nuzulack Dausen

Nuzulack Dausen ni Mkuu wa dawati la habari za takwimu wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti. Mwaka 2015 alishinda tuzo ya Mwandishi bora wa habari za Uchunguzi kwa upande wa magazeti zinazotolewa na Baraza la Habari Tanzania (MCT). Amejikita zaidi katika habari za biashara, uchumi, teknolojia na data.

MWANANCHIDataLab by Code for Tanzania