Vifo vya watoto njiti pasua kichwa Afrika Mashariki

Maria Mtili
December 12, 2017

Herieth Makwetta, Mwananchi

Wakati nchi zinazoendelea zikipambana na vifo vya wajawazito, makumi ya watoto njiti wanafariki kila siku katika hospitali na vituo vya afya vilivyopo maeneo mbalimbali Tanzania, Uganda na nchini Kenya.

Ripoti iliyochapishwa 2012 na jopo la wataalamu wawakilishi wa mashirika makubwa ya kimataifa duniani, wasomi, taasisi za kitaaluma na mashirika ya Umoja wa Mataifa, makadirio yanaonyesha uzito wa tatizo la watoto njiti ni kubwa kuliko ilivyoripotiwa mwaka 2010.

Japokuwa vizazi kabla ya muda ni taswira ya tatizo la kidunia, lakini nchi zenye uchumi mdogo hasa zile za Afrika na za Kusini mwa Jangwa la Sahara zinaelemewa na tatizo hilo.

Miongoni mwa nchi 11 zenye viwango vya juu vya kuzaliwa watoto njiti isipokuwa mbili tu, zipo Kusini mwa Jangwa la Sahara kwa mujibu wa ripoti ya mwaka 2010.

Tanzania

Nchini Tanzania takwimu zinaonyesha asilimia 13 ya watoto huzaliwa wakiwa na uzito pungufu ambao huchangia kwa asilimia 86 ya vifo vya wachanga.

Ripoti ihiyo inasema tatizo linalochangia kusababisha vifo vya watoto hao linalokadiriwa kufikia asilimia 27 ya vifo hivyo, ni pamoja na mtoto kuzaliwa njiti, maradhi ya vimelea vya bakteria, matatizo ya kupumua na kuvuja damu.

Kila mwaka, zaidi ya watoto 210,300 wanazaliwa kabla ya kutimiza wiki 37 za ujauzito na kati yao, zaidi ya watoto 13,900 hufariki dunia. Kwa takwimu za mwaka 2016 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili pekee, inaonyesha idadi hiyo imeongezeka maradufu kutoka 30 mwaka 2012 hadi kufikia 1,500 mwaka 2016.

Mkuu wa Kitengo cha Watoto Njiti wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Edna Majaliwa anasema licha ya ukubwa wa tatizo, huduma ya Kangaroo imesaidia kwani ukaribu wa ngozi kwa ngozi baina ya mama na mtoto husaidia kupata joto asilia na lisilobadilika kirahisi.

Alisema husaidia pia kupunguza maambukizi ya maradhi kwa watoto, kuongeza hali ya kunyonyeshwa, kupunguza kupaliwa kwa maziwa kunakosababishwa na vifo vya ghafla na upatikanaji wa taarifa ya haraka pindi hali ya mtoto inapobadilika.

Hata hivyo, Dk Majaliwa anasema takwimu zinaonyesha vifo vya watoto njiti vimeendelea kupungua katika kipindi cha miaka mitano kuanzia 2012 hadi 2017 kwa Muhimbili.

“Hii inatokana na jitihada mbalimbali zinazofanywa na wadau wa afya ikiwamo kuanzishwa kwa huduma ya Kangaroo katika hospitali za mikoa na rufaa na upatikanaji wa huduma za dharura za kujifungua kwa wajawazito kwenye vituo vya afya (EmONC),” anasema.

Wanakabailiana vipi na changamoto

Hata hivyo anasema kuna changamoto kadhaa hasa ya ongezeko la watoto njiti linalosababisha kuwapo kwa ufinyu wa nafasi na huduma.

Kuhusu Incubator, Dk Majaliwa anasema Muhimbili ziko chache , lakini kutokana na uwapo wa watoto wengi wanaohitaji huduma hiyo, haziwezi kutumika, hivyo vyumba vya watoto njiti vimeongezwa joto kama la incubator ili kuweza kuwahudumia wote .

Kwa mujibu wa Msemaji wa Bohari ya Dawa (MSD), Etty Kusiluka mashine za incubator hazihifadhiwi katika maghala ya bohari, bali MSD huziagiza kama kuna hospitali inazihitaji.

“Kuna baadhi ya vitu ni nadra kuvinunua hasa vifaa tiba kama incubator, hata hivyo bei yake inategemeana na mteja ambaye tunakwenda kununua kuna kampuni mbalimbali zinatengeneza, lakini katika rekodi yetu incubator ya mwisho ilinunuliwa kwa Sh3.37 milioni,” anasema Kusiluka.

Kenya

Nchini Kenya, takribani watoto njiti 26 wanazaliwa kila siku, wakati huohuo 8,303 kati yao hufariki dunia kabla ya mwezi mmoja wa maisha yao kila mwaka.

Mratibu Mwandamizi wa Afya wa Shirika la Save The Children la Jijini Nairobi, Joan Emoh aliliambia Mwananchi tatizo la watoto kuzaliwa njiti limeongezeka kwa muongo mmoja sasa.

Lakini anasema juhudi mbalimbali zinahitajika ili kutimiza malengo ya milenia ya mwaka 2030, yanayotaka kufikia watoto 12 kati ya 1,000 wanaozaliwa njiti wawe wanaishi.

Akizitaja takwimu za mwaka 2015, alisema watoto njiti 188,900 walizaliwa nchini humo, sawasawa na watoto wanane wanaozaliwa, mmoja wao ni njiti.

“Tunaposema mtoto njiti wametofautiana pia katika ukubwa wa tatizo, kitakwimu tukifuatilia, kati ya njiti 16, mmoja amezaliwa kabla ya wiki 10, wawili kabla ya wiki 6 mpaka 10 na 16 mara nyingi wanazaliwa kabla ya wiki moja mpaka sita,” anasema Joan.

Hata hivyo anasema kifo kimoja cha mtoto njiti kati ya vine, husababishwa na matatizo yatokanayo na kuzaliwa kabla ya wakati.

Joan anasema lazima ipatikane mbinu mbadala, ili kuepuka watoto wengi kutumia incubator moja, ambayo inaweza kusababisha maambukizi na vifo vingi vya watoto hao.

Kwa mujibu wa Dailymonitor la nchini Uganda, watoto njiti huchangia asilimia 25 ya watoto wote wanaofariki dunia baada ya kuzaliwa ambao ni sawa asilimia 13 ya watoto kwa kila vizazi hai 1,000.

Takwimu hizo zinaiweka nchi ya Uganda kwenye nafasi ya 28 kidunia zinazoongoza kwa vifo vya watoto njiti kwa mujibu wa ripoti ya Shirika linaloshughulikia watoto duniani (Unicef) iliyotolewa hivi karibuni. Ripoti hiyo inaeleza Uganda inapoteza watoto njiti 45,000 kila mwaka.

Teknolojia mpya

Teknolojia mpya ya kuwatunza watoto waliozaliwa kabla ya wakati kwa blanketi maalumu ‘incubator blanket’ imeelezwa itaokoa maelfu ya wanaozaliwa kabla ya wakati Afrika.

Ugunduzi huo umetambulishwa baada ya American firm Warmilu Inc iliyopo jijini Nairobi kubuni blanketi maalumu ambalo ni rahisi na rafiki kwa mama kumtunzia mtoto.

Teknolojia hiyo inayojulikana ‘IncuBlanket’, imeleta uvumbuzi katika utegemezi wa incubator za kutumia umeme na huduma ya Kangaroo ambayo hutolewa na mama (Kangaroo Mother Care). Imeelezwa huduma ya kifaa hicho itafanana na joto la mama.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Warmilu, Grace Hsia, teknolojia hiyo itaweza kuokoa maelfu ya maisha ya watoto njiti hususan maeneo ya vijijini kuliko na matatizo ya umeme na baadhi ya vituo vya afya visivyoweza kumudu gharama za incubator.

Utafiti wa Shirika la Afya Duniani (WHO) watoto milioni 20 wanazaliwa kila mwaka duniani, kati yao milioni 4 huzaliwa kabla ya muda wao ‘njiti’ na vifo vingi vimetajwa kutokea katika nchi zinazoendelea,c takribani milioni moja kati yao hufariki dunia kwa kukosa huduma muhimu.

Takwimu za Tanzania

Takwimu za tangu mwaka 2012 za watoto wachanga wanaolazwa Muhimbili, kati ya yao, asilimia hizo ni wale waliozaliwa kabla ya muda yaani ‘njiti’

Mwaka Takwimu

2012-2013 40.9%

2013-2014 29.4%

Maria Mtili

MWANANCHIDataLab by Code for Tanzania